كِتَابُ الزَّوَاجِ
Kitabu Cha Ndoa
النُّشُوْزُ وَعِلَاجُهُ
Uasi Wa Mke Kwa Mume Na Njia Za Kuutibu
05: Mvutano Kati Ya Mke Na Mume Na Utatuzi Wake:
Ikiwa mgogoro na msuguano utajitokeza kati ya wanandoa, basi itabidi wapelekwe waamuzi wawili wa kutafuta suluhu kati yao na kuwaasa kama Alivyoamuru Allaah Ta'aalaa.
Mwamuzi mmoja atatoka upande wa mume na mwingine upande wa mke. Kwa kuwa kuendelea mvutano kati yao, kutapelekea ndoa kuvunjika, watoto watasambaratika na mahusiano kati yao wawili yatakatika na hata kwa jamaa zao.
Allaah Subhaanahuu wa Ta'aalaa Amesema:
"وَإِنْ خِفْتُمْ شِقَاقَ بَيْنِهِمَا فَابْعَثُوا حَكَمًا مِّنْ أَهْلِهِ وَحَكَمًا مِّنْ أَهْلِهَا إِن يُرِيدَا إِصْلَاحًا يُوَفِّقِ اللَّـهُ بَيْنَهُمَا ۗ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَلِيمًا خَبِيرًا "
"Na mkikhofu mafarikiano baina yao wawili, basi pelekeni mwamuzi kutoka watu wa mume na mwamuzi kutoka watu wa mke. Wakitaka sulhu, basi Allaah Atawawafikisha baina yao. Hakika Allaah daima Ni Mjuzi wa yote, Mwenye upeo wa khabari za dhahiri na za kufichika". [An-Nisaa: 35]
Waamuzi hawa wanatakikana wafanye juhudi kubwa katika zoezi hilo la kuleta suluhu na kuondosha mfarakano, wawe wakweli, wamwelekeze vyema mwenye makosa kati yao, na wamkinaishe akubali haki.
Mamlaka Ya Waamuzi Wawili:
Ikiwa waamuzi hawa (wapatanishi) watafanya wawezavyo kwa ajili ya kuleta suluhu kati ya mke na mume lakini wakakuta kwamba hilo haliwezekaniki, je, watakuwa na mamlaka ya kuwaachanisha? Au ni lazima warejee kwa mke na mume (kusikia uamuzi wao)? Kuhusiana na hili, kuna kauli mbili za 'Ulamaa:
Kauli iliyo sahihi zaidi ni kuwa waamuzi hawa si wawakilishi bali ni sawa na makadhi wawili. Na kwa muktadha huo, watakuwa na mamlaka ya kuwaachanisha, ni sawa watake au wasitake, au hata bila kupata amri kutoka kwa kadhi mkuu. Haya ni madhehebu ya Maalik, Ahmad na baadhi ya 'Ulamaa wa Kishaafi'iy, na ni chaguo pia la Sheikh wa Uislamu.
Dalili zao ni:
-
Neno Lake Ta'aalaa:
"فَابْعَثُوا حَكَمًا مِّنْ أَهْلِهِ وَحَكَمًا مِّنْ أَهْلِهَا"
"Basi pelekeni mwamuzi kutoka watu wa mume na mwamuzi kutoka watu wa mke". [An-Nisaa: 35]
Wanasema: "Haya ni Maneno ya Allaah Ta'aalaa yanayomaanisha kwamba hao ni mahakimu (waamuzi) wawili na si wawakilishi. Hakimu na mwakilishi ni watu wawili tofauti kabisa katika msamiati wa kisharia. Na Allaah Anapompambanua kila mmoja na mwingine, basi haitakikani maana moja kupandishwa juu ya nyingine. Hivyo basi, kufanya hivyo kunazingatiwa kama ni uchakachuaji na upotoshaji wa hukumu". ["Ahkaamul Qur-aan" cha Ibn Al-'Arabiy (1/424).
2. Neno Lake Ta'aalaa:
"إِن يُرِيدَا إِصْلَاحًا"
"Wakitaka sulhu ". [An-Nisaa: 35]
Wanasema: "Wawili wanaokusudiwa hapa ni waamuzi wawili, na si mke na mume. Na kwa hivyo, ridhaa ya mke na mume haizingatiwi hapa, na kwamba waamuzi hao wana haki ya kuamua lolote nje ya matakwa ya mke na mume. Na kama wangekuwa ni wawakilishi, basi utashi wa maamuzi ungelikuwa ni utashi wa mke na mume". [Tafsiyr Al-Qurtubiy (5/175) na Zaadul Ma'aad (4/33)]
3. Toka kwa 'Ubaydah, amesema:
"جَاءَ رَجُلٌ وامْرَأَةٌ إِلَى عَليِّ بنِ أَبِي طَالِبٍ وَمَعَ كُلٍّ واحِدٍ منْهُمَا فِئَامٌ من النَّاسِ، فَأَخْرَجَ هؤلاء حَكَمًا و هؤلاء حَكَمًا، فَقَالَ عَليٌّ للحَكَمَيْنِ: أَتَدْرِيَانِ مَا عَلَيْكُمَا؟ إِنْ رَأَيْتُمَا أَنْ تَجْمَعَا جَمَعْتُمَا، فَقَالَ الزَّوْجُ: أَمَّا الفرقة فَلَا، فَقَالَ عليٌّ كَذبتَ، والله لا تَبْرَحُ حتَّى تَرْضى بِكِتَاب الله لَكَ وعَليْكَ، فَقَالَتِ المرْأَةُ: رَضِيْتُ بِكِتَابِ الله تعالى لي وعليَّ"
"Mume na mkewe walikuja kwa 'Aliy, huku kila mmoja kati yao akiwa na kundi kubwa la watu. Kundi moja likatoa mwamuzi na kundi jingine pia. 'Aliy akawauliza waamuzi hao wawili: Je, mnajua nini mnapaswa kufanya? Mkiona kuwatenganisha ni sawa, basi watenganisheni, na ama mkiona kuwabakisha waendelee na ndoa yao, basi wabakisheni. Mume akasema: Kama ni kutenganishwa, hilo hapana. 'Aliy akamwambia: Mwongo wee. Wa-Allaah, huondoki hapa mpaka uwe umeiridhia Hukmu ya Allaah, ni sawa iwe upande wako au dhidi yako. Na mwanamke akasema: Nimeiridhia Hukmu ya Allaah iliyo upande wangu au iliyo dhidi yangu". [Isnaad yake ni swahiyh. Imechakatwa na 'Abdul Razzaaq (6/512), Al-Baghawiy kwenye "Sharhu As-Sunnah" (9/190), An-Nasaaiy katika "Al-Kubraa" (4678), Sa'iyd bin Mansour (628), Ash-Shaafi'iy (655) na Al-Bayhaqiy (7/305)]
4. Ulipotokea ugomvi kati ya 'Aqiyl bin Abiy Twaalib na mkewe Faatwimah bint 'Utbah, bibi huyu alipeleka mashtaka yake kwa 'Uthmaan (Radhwiya Allaah 'anhu), na 'Uthmaan akawapeleka Ibn 'Abbaas na Mu'aawiyah kuwa waamuzi kati yao. Na Ibn 'Abbaas akasema: "Lazima nitawaachanisha tu". [Isnaad yake ni swahiyh. Imechakatwa na At-Twabariy (5/74), 'Abdul Razzaaq (6/513) na Ash-Shaafi'iy]
Na kwa muktadha wa haya, ni haki kwa waamuzi hawa wawili kutoa talaka kwa niaba ya mume, au kupitisha khul-'u (mke ajivue ndoa kwa kumlipa mume fidia) kwa niaba ya mke, na hukumu yao inapita moja kwa moja. Na Allaah Ndiye Ajuaye zaidi.
Na ikiwa waamuzi hawa watakhitilafiana, kwa mfano, mmoja wao akatoa talaka moja na mwingine mbili (kwa wale wenye kusema zinapita), au mmoja wao akapitisha khul-'u kwamba mke amlipe mume shilingi 1000 na mwingine akasema 2000 na mfano wa hivyo, katika hali hii, hukumu yao haitopita, bali kadhi atapeleka waamuzi wengine wawili wapya mpaka wakubaliane uamuzi mmoja.
Na ikiwa kadhi hatopata toka kwa jamaa za mke na mume watu wanaofaa kuwa waamuzi, Jumhuwr ya 'Ulamaa wamejuzisha katika hali hii kupeleka waamuzi wawili wasio na mahusiano ya kidugu na mke na mume, na hukumu yao itapita kama watakubaliana. [Fat-hul Qadiyr (3/223), Mawaahibul Jaliyl (4/27), Mughnil Muhtaaj (3/261) na Sharhu Muntahaa Al-Iraadaat (3/206)]